TANZANIA MWENYEJI WA MAADHIMISHO YA MIAKA 20 YA BARAZA LA AMANI NA USALAMA LA UMOJA WA AFRIKA


Na Mwansdishi wetu,HabariPlus

RAIS wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluhu Hassan anatarajiwa kuongoza maadhimisho ya miaka 20 ya baraza la amani na usalama la umoja wa Afrika yatakayofanyika Mei 25, katika ukumbi wa Mikutano wa Kimataifa wa Julius Nyerere.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki January Makamba amesema kuwa ni heshima kubwa Tanzania kuwa mwenyeji wa maadhimisho hayo ambapo wageni 120 wanatarajiwa kuhudhuria kutoka nchi mbalimbali.

Amesema kuwa, Tanzania kuongoza maadhimisho hayo ni heshima kubwa kwani ni nchi 15 tu kati ya nchi 55 ambazo ni wanachama wa Umoja wa Afrika, ndio wajumbe wanaounda baraza la amani na usalama la umoja wa Afrika.

"Nchi ambazo zina wajumbe wa baraza hilo ni Tanzania, Uganda na Djibouti (kutoka Ukanda wa Mashariki), Cameroon, DRC na Equatorial Guinea (Kanda ya Kati), Afrika Kusini, Angola na Botswana (Kanda ya Kusini), Cote d’Ivoire, Gambia, Nigeria na Sierra Leone (Magharibi) na Misri na Morocco (Ukanda wa Kaskazini)".

"Nipende pia kuwataarifu kuwa pamoja na kuwa wajumbe, mwezi huu wa Mei 2024, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imepewa jukumu jingine kubwa zaidi,  tumeaminiwa kuwa Mwenyekiti wa baraza hili kwa mwezi Mei, hivyo, tukiwa wenyekiti tunalo jukumu kubwa la kusimamia shughuli zote zinahusu baraza, ikiwemo kufuatilia kwa karibu hali ya ulinzi na usalama kwenye bara la Afrika"

Aidha amesema katika kuelekea maadhimisho hayo Tanzania kwa kushirikiana na sekretarieti ya baraza hilo waliandaa ratiba ya shughuli mbalimbali ndani ya mwezi huo ambapo wiki ya kwanza itahusu usuluhishi na majadiliano, wiki ya pili ilihusu masuala ya mahitaji ya kibinadamu, amani na usalama, wiki ya tatu ilihusu wanawake na vijana katika amani na usalama na wiki ya nne ulinzi kwa watoto na wiki ya tano ilihusu kusaidia misheni za amani.

Amesema kuwa, miongoni mwa watu mashuhuri watakaoshiriki maadhimisho hayo ni Mhe. Jessica Alupo, Makamu Rais wa Uganda; Mhe. Moussa Faki Mahamat, Mwenyekiti wa Kamisheni ya Umoja wa Afrika, Rais Mstaafu wa Nigeria, Mhe. Olesegun Obasanjo, Rais Mstaafu Burundi, Mhe. Domitien Ndayizeye, Rais Mstaafu wa Msumbiji, Mhe. Joachim Chissano na Mhe. Rais Mstaafu Mhe. Jakaya Mrisho Kikwete. 

Aidha, katika kusherehekea Maadhimisho hayo, tarehe 24 Mei, 2024 kutafanyika mjadala wa wazi kwenye Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ili kupokea maoni yao kuhusu utendaji kazi wa baraza na namna ya kuweza kuliimarisha, kwani katika kipindi cha miaka 20 ya uhai wa baraza hilo limepata mafanikio katika kuimarisha amani na usalama Barani Afrika. 

"Kwa muktadha huo, nawakaribisha wananchi kujitokeza kwa wingi kwenye Mjadala Chuo Kikuu cha Dar es Salaam ili kutoa maoni yao, aidha, nawahimiza wadau wote walioalikwa kushiriki kwenye kilele cha maadhimisho tarehe 25 Mei 2024"amesema Waziri Makamba.

Katika hatua nyengine, amempongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kazi kubwa anayofanya ya kuimarisha diplomasia ya nchi na kuiongoza nchi katika kutoa kipaumbele kwenye masuala ya ulinzi na usalama katika bara la Afrika na dunia kwa ujumla.  

Baraza la Amani na usalama ni chombo cha juu kabisa cha maamuzi kuhusu masuala ya amani na usalama kwenye umoja wa Afrika, ambapo miongoni mwa majukumu ni pamoja na kuzuia kutokea kwa migogoro, kusuluhisha au kukabiliana nayo pale inapojitokeza na kutoa miongozo ya kushughulikia masuala ya kiusalama.


Comments

Popular posts from this blog

TMA YATOA TAHADHARI KUHUSU UWEPO WA KIMBUNGA "HIDAYA"

HUU HAPA MWENENDO WA KIMBUNGA "HIDAYA" , UPEPO KUVUMA KWA KASI YA KILOMITA 130 KWA SAA

NHIF YAFANYA MABORESHO YA KITITA CHA HUDUMA ZA MATIBABU, YAENDELEA KUPOKEA MAONI