TAASISI YA MAMA ONGEA NA MWANAO YATOA VITI MWENDO 250 KWA WATOTO WENYE UHITAJI


Taasisi ya Mama Ongea na Mwanao kwa kushirikiana na wadau wa maendeleo wametoa msaada wa viti mwendo 250 kwa ajili ya watoto wenye uhitaji maalum ambavyo vitawasaidia kutimiza ndoto zao za kupata elimu.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam Mwenyekiti wa Taasisi hiyo Steve Nyerere amesema kuwa kampeni hiyo ya kugawa viti mwendo kwa watu wenye mahitaji maalum ni juhudi za kuunga mkono jitihada za Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt Samia Suluh Hassan katika kuhakikisha watoto wote wanapata elimu.

Amesema kuwa, kuna baadhi ya wazazi wamekuwa wakipitia wakati mgumu mara baada ya kujifungua watoto wa aina hiyo kwani hutelekezwa na waume zao.

"Kuna wanaume ni wazembe katika kulea watoto wenye ulemavu ambapo hufikia kusema watoto hao sio wa kwao na kuwatelekeza, kuwaacha katika mazingira magumu"amesema Steve.

Ameongeza kuwa, mtoto kuzaliwa na hali ya ulemavu haimzui kupata haki yake ya msingi ya kupata elimu bora kwani kupata mtoto mwenye hali hiyo ni mipango ya Mwenyezi Mungu, hivyo wana haki sawa kama watoto ambao wamezaliwa bila ulemavu.

"Naomba jamii iondoe dhana potofu juu ya mtoto mwenye ulemavu hasa wanaume maana hawa ndio wamekua wakiwatelekeza sana, sisi kama taasisi tupo tayari kupeleka msaada popote hivyo tunaomba na wadau wengine watuinge mkono"amesema Steve.

Kwa upande wake Katibu wa Taasisi ya Mama Ongea na Mwanao,  Evon Sherry (Monalisa)  amesema taasisi hiyo imetembelea mikoa mitano na kubakisha mikoa miwili kwa jili ya viti mwendo kwa wahitaji.

Amesema kuwa, kampeni ya "Baskeli ya shule ya Mama" inalenga kumsaidia mtoto mwenye uhitaji kupata elimu, hivyo watahakikisha wanawafikia watoto wengi ili waweze kutimiza ndoto zao.

"Rais Dk.Samia Suluhu Hassan anawasaidia wakina mama katika sekta mbalimbali ikiwemo afya,  maji na nishati lakini sisi tumeamua kumtua mama mtoto mgongoni"amesema Evon

Comments

Popular posts from this blog

TMA YATOA TAHADHARI KUHUSU UWEPO WA KIMBUNGA "HIDAYA"

HUU HAPA MWENENDO WA KIMBUNGA "HIDAYA" , UPEPO KUVUMA KWA KASI YA KILOMITA 130 KWA SAA

NHIF YAFANYA MABORESHO YA KITITA CHA HUDUMA ZA MATIBABU, YAENDELEA KUPOKEA MAONI